Habari mpya

WAPARE NA UPARE "Je waijua asili ya wapare...???"


NA Ramadhani Gidioni.
Tanzania ni nchi yenye makabila zaidi ya 120 lakini katika makala hii nitachambua kabila la wapare, je wapare ni kina nani?  Asili yao ni nini? Wanaishi wapi? Wanajishughulisha na nini? Lakini pia ni zipi mila na desturi zao?
Kabila la wapare linapatikana mkoani Kilimanjaro kaskazini mwa Tanzania katika wilaya ya Same na Mwanga japo wapo wapare wanaoishi maeneo ya Moshi kama vile chekereni,himo,uchira, mabungo na moshi mjini, vilevile  wilayani Hai kwenye maeneo kama Rundugai na mto weruweru.Mkoani Tanga wapare wanaishi zaidi lushoto katika maeneo ya Bumbuli na Mavumo.
Asili ya wapare inasemekana ni Taveta nchini Kenya ambako waliishi huko zaidi ya karne moja na nusu iliyopita wakijulikana kwa jina la “waasu” wakitumia lugha iliyojulikana kama “chasu” kabla ya kuingia Tanganyika kupitia mpaka wa Taveta.Historia inaeleza kuwa wapare wa mwanzo walifikia katika miteremko ya mlima kilmanjaro wakiongozwa na machifu wao mashuhuri kama vile mfumwa (chief)  Boazi Mashambo ambako waligombana na wenyeji waliowakuta maeneo hayo ambao ni wachaga waliowafukuza kutoka katika aridhi yao hatimaye walihamia milima ya Same na Mwanga ambayo saivi inafahamika kama milima ya upare.
Image result for upareni
Wapare wamegawanyika katika makundi mawili wapo wapare wa kaskazini maarufu kama “vampare va mpare ya ughu” kwa lugha ya kipare wakimaanisha wapare wa upande juu hawa huishi wilayani Mwanga kwenye meneo ya ugweno ambao huongea lugha ijulikanayo kama “kigweno” na wapo wanaishi maeneo ya Usangi hawa hutumia lugha ya kipare. Kundi la pili ni wapare wa kusini “vampare va mpare ya kusea”,wakimaanisha wapare wa upande wa chini hawa huishi wilayani Same huzungumza kipare jopo kinatofutiana matamshi (lafudhi) na wapare wa usangi.
Kabila hili hujihusisha zaidi na kilimo cha mahindi,maharagwe, mpunga, na vitunguu hasa kwenye mabonde maarufu yaliyojaliwa maji na rutuba kama vile bonde la Ruvu,kisiwani, maore na Ndungu wilayani Same vilevile maeneo ya Ugweno na Usangi wilayani Mwanga ambapo kilimo cha migomba kimeshamiri zaidi.Same milimani pia kwenye maeneo ya Mbaga,vudee,chome na Gonja kilimo cha migomba na nafaka kama maharagwe na mahindi hutegemewa zaidi kama zao la chakula katika maisha ya kila siku.Katika eneo la mamba miamba na Kanza husifika zaidi kwa kilimo cha tangawizi pia yapo mabwawa na madimbwi mbalimbli yatumikayo katika shughuli za uvuvi kama vile bwawa la nyumba ya mungu, bwawa la ndungu na dimbwi la msangeni.
Vile vile wapare wa mwanzo walijihusisha na shughuli za uwindaji hasa waliokua wakiishi maeneo ya tambarare kama vile Igoma,Njiro, Maore, Kisiwani, Mpirani ,Ndungu pamoja na maeneo mengine wakati wapare wamilimani walijikita zaidi katika shughuli za kilimo pia zipo koo za kipare zilizojishughulisha na ufuaji wa chuma tangu karne ya 18,  ukoo uliojikita zaidi na shughuli hizo ni Washana waliozalisha vifaa mbalimbali vya chuma kama vile majembe,mashoka, visu, mishale na mapanga vilivyo tumika katika biashara na makabila ya jirani kama vile wachaga na wasambaa.
Mbali na uwepo wa aridhi nzuri yenye  rutuba kwa kilimo katika milima na mabonde ya upare pia vipo vivutio vya utalii wa asili katika maeneo hayo ikiwemo mito maarufu kama vile Hingilili,Rika,Nakombo, Mhoke vuta, Yongoma, Mwetanano pamoja na maporomoko yanayosemekana kuwa marefu kuliko ya ziwa Victoria  maarufu kama “Ndurumo” yapatikanayo eneo la Gonja bombo.
Image result for maporomoko ya maji upareni
Pia ipo misitu mikubwa ya asili kama vile Shengena ambao unasemekana ni msitu wa pili kuleta hali ya hewa nzuri duniani baada ya Amazon,msitu wa Ngagheni Mpinji unaopatikana vudee unaoaminika kutumiwa katika mila za kipare na matambiko kati ya karne ya 17 na 19.
Image result for ndungu upareni
                                                           msitu wa shengena.
Lakini pia upo msitu wa Wambughu uliopo karibu na kijiji cha Dangaseta amboko moja ya koo za kipare kwa jina Wambughu ambao wengi huishi Lushoto  mkoani Tanga hutambika katika moja ya muembe uliopo ndani ya msitu huo, hata hivyo upo msitu na chanzo cha maji ya Kwachengo ambayo ni maji ya ajabu yanayotiririka kutoka chini kwenda juu.

                                                             IImage result for ndungu upareni
                                                               image/ndungu.com
Hali kadhalika upareni kuna hifadhi kubwa ya Taifa inayojulikana kama Mkomazi,Bwawa la Kalimawe na Nyumba ya mungu,milima ya Kindoroko,mokanda  na Masheko vudee ndolwa.Pia kuna majabali makubwa yavutiayo wataalii kuja kutizama kama lile la Malameni linalopatikana Mbaga Manka ambalo zamani inasemekana zilikua zikisikika sauti za wasichana watatu ndani ya jiwe hilo zikizungumza, hata hivyo kuna jabali la Mhewe linalopatikana vudee ndolwa,jiwe la mkumba vana,Ikamba, Mfinga na Lubegho linalopatikana Usangi.
Mzee eliapendavyo  Elisa Mruth ni miongoni mwa wazee wa kipare wanaoifahamu vyema historia ya kabila la wapare ambako alisema kuwa mila na desturi za wapare zinasisitiza mafundisho mema miongoni mwa vizazi vyote kwani wapare ni kabila lenye historia ya kupenda haki,heshima, upendo na amani katika jamii.Alisema zamani vijana wa kipare walipofikia umri wa kubalehe walipewa mafundisho maalumu ya kimila yaliyojuikana kama “maluthumo”  ambapo vijana wa kiume walitenganishwa na wakike katika misitu maalim iliyojulikana kama “mshitu wa mtatho” wakimaanisha msitu wa ibada, wavulana walipewa mafundisho yajulikanayo kama “ngathu ya mshitu” na wasichana walifundishwa katika mafunzo ya yaliyojulikana kama “kieko” walipofundishwa jinsi ya kutengeneza familia bora na kuheshimu wazazi na jamii nzima.
Wanawake walipojifungua walipongezwa kwa sherehe maalum zilizoitwa “mchumbi” ambazo waliletewa zawadi mbalimbali na wanawake wenzao katika vikapu vilivyofungwa na vitambaa kama kaniki.Zawadi hizo mara nyingi zilikuwa asali,ndizi zilizokaushwa zilizojulikana kama “makafi”,maziwa,mahindi pamoja na mihogo ya kukausha.Sherehe hizi za wanawake zinafanyika mpaka leo katika kaika mila za wapare ambapo zawadi kama sukari,mahindi,maharagwe na mafuta ya kupikia hupendelewa zaidi kwa sasa.
Image result for maporomoko ya maji upareni
Vijana wa kipare pia waliweza kuyatunza mazingira yanayowazunguka kutokana na mafundisho na misemo iliyojaa hekima waliopewa na wazee katika koo zao kwa mfano walifundishwa kutunza vyanzo vya maji wakiamini misemo ya wazee wao waliowaita “vakaka” waliosema kuwa wakijisaidia kwenye maji maziwa (matiti) ya mama zao yatakatika.
Misemo ya wazee iliwasaidia kuwa na nidhamu,upendo na mshikamano ,maneno kama “chambi ni kuonjanya” yakiwa na maana umoja ni mshikamano yaliwapa ujasiri wakufanya kazi kwa pamoja na kwa upendo.
Aidha mzee Mruth amesema kuwa mwanzoni kabla ya ujio wa waarabu na wamishenari amboko dini za uislamu na ukristo zilikua hazijafika katika jamii za wapare watoto walipewa majina kutokana na matukio maalumu wakati mototo wanapozaliwa mfano mototo wa kiume aliyezaliwa wakati wa vita aliitwa Senkondo wakati wakike aliitwa Nankondo,mathalalani watoto waliozaliwa wakati wa mvua waliitwa “Nambua” wakati wakati wa usiku waliitwa “nakio” na hata waliozaliwa wa wakati wa shida kama vile njaa waliitwa majina yanayoshabihiana na wakati huo mfano “Senzota”, nzota ikiwa na maana ya njaa.
Pia majina ya maeneo mbalimbali yalitokana na majina ya koo za kipare zinazoishi maeneo hayo mfano maeneo kama Chome wanaishi  ukoo wa wachome,Gonja wanaishi wagonja, Mbaga wanaishi wambaga,ugweno wanaishi wagweno na maeneo mengine mingi yalipewa majina kwa misingi hiyo.
Hata hivyo mila na desturi za wapare zimebadilika sana katika miaka ya hivi karibuni  kutokana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia,maendeleo ya utandawazi, elimu ya magharibi pamoja na mafunzo ya dini yaliyobadilisha imani za watu katika kabila hilo hali iliyopekea kuacha kabisa ibada zao na mitambiko katika misitu mikubwa na majabali na kujikuta wakifwata maandiko ya msaafu na bibilia ya kuabudu mungu katika makanisa na misikiti.

Na Ramadhani Gidion.

UDSM-SJMC

No comments

+255716829257