Habari mpya

KENYA: UTATA SHAMBULIZI LA KITUO CHA POLISI..

 
Utata umetanda kuhusu nani hasa aliyeshambulia maafisa wa polisi katika kituo cha polisi cha Kapenguria, kaskazini magharibi mwa Kenya.
Mshambuliaji huyo alikabiliana na maafisa wa polisi kwa karibu zaidi ya saa sita mnamo Alhamisi.
Maafisa kadha wa polisi waliuawa.
Taarifa kutoka kwa mkuu wa polisi Joseph Boinnet ilisema mshukiwa wa ugaidi aliyekuwa amekamatwa na kuzuiliwa alimpokonya silaha afisa wa polisi na kuwafyatulia risasi maafisa waliokuwa kwenye zamu mwendo wa saa kumi na moja alfajiri.
"Juhudi zake za kutaka kutoroka zilizimwa na maafisa wengine waliofika upesi, na wamezingira kituo,” alisema.
"Tumetuma kikosi cha maafisa maalum wa kuokoa mateka kusaidia kuokoa mahabusu walio seli na kudhibiti hali.”
Kamishna wa Jimbo la Pokot Magharibi Wilson Wanyanga amenukuliwa na gazeti la Daily Nation la Kenya akisema mkuu wa polisi wa kituo hicho ni miongoni mwa waliouawa.
Taarifa za awali katika vyombo vya habari Kenya zilikuwa zimedokeza kwamba shambulio hilo lilitekelezwa na watu waliotaka kumuokoa mshukiwa aliyekuwa kizuizini.
Baadaye, polisi walisema ni mshukiwa mwenyewe aliyempokonya afisa wa polisi risasi na akawafyatulia risasi polisi akijaribu kutoroka.
Lakini baadhi ya taarifa zinasema anayeaminika kuwa mshambuliaji alikuwa afisa wa polisi aliyetaka kumwachilia huru mshukiwa huyo.
Mshambuliaji aliripotiwa kupigwa risasi baadaye adhuhuri.
Mshukiwa huyo wa ugaidi ametambuliwa kama Omar Okwaki Eumod ambaye taarifa zinasema alikuwa amepangiwa kufikishwa kortini Alhamisi asubuhi

No comments

+255716829257