Habari mpya

ZIJUE ATHARI ZA MALEZI YA KIBAGUZI KWA MTOTO ASIYE WA DAMU.



 
Mtoto yeyote ana haki kisheria awe ni yatima, mlemavu au anaishi mbali na wazazi wake. Ikiwa ni kuthaminiwa na kupatiwa mahitaji yote ya msingi, kama vile elimu, matibabu, chakula bora, kucheza, kupumzika, kutoa maoni na kuskilizwa pasipo kubaguliwa kwa namna yoyote.
Leo tunaangalia malezi ya watoto ambao siyo wa damu yako (yaani si wa kwako wa kuzaa), wanaweza kuwa wa ndugu zako au la.
Yamkini unaishi nao kutokana na wao kufiwa na wazazi, wazazi wao kutokuwa na nafasi ‘kihali’ kuwahudumia au sababu fulani ambazo zimepelekea wewe kuwa mlezi wao. Kuna tabia zimejengeka katika jamii juu ya malezi ya watoto wanaolelewa na walezi wa namna hii.
Watoto hawa wamekuwa wakiishi katika mazingira magumu kwa kunyimwa haki zao za msingi, kufanyishwa kazi ngumu bila kujali umri na uwezo wao, kutokupelekwa shule, kutukanwa matusi, kunyimwa chakula na kadhalika kwa kigezo kuwa si watoto wa kuwazaa.
 Hili hufanyika wakati walezi hawa wakiwapatia malezi bora na mahitaji yote watoto wao wa kuwazaa! Hii ni mbegu ya kibaguzi, ubaguzi wa ‘nafasi’ kimaisha!
Watoto hawa huamshwa majogoo kuteka maji, kufua nguo za watu wote nyumba nzima, kuosha vyombo na kusafisha nyumba wakati watoto wa mlezi wao wakiwa wamechapa usingizi.
Yaani mtoto anakuwa mtumwa na akikosea kidogo hupigwa na kuumizwa hivyo kukosa raha kabisa. Watoto namna hii hukimbilia mitaani na kuhatarisha maisha yao zaidi.
 Tafiti zinaonyesha kuwa watoto wengi waishio na kufanya kazi mitaani nchini Tanzania hutokana na malezi ya unyanyasaji waliyoyapata kutoka kwa wazazi ama walezi wao na hivyo kukimbilia mitaani ili kupata amani.
Pia tafiti zinzonyesha kuwa watoto wanaolelewa namna hii hujengewa chuki yenye kudumu mioyo mwao kwa muda mrefu na aghalabu hujenga nia ya kulipiza kisasi kwa waliowatendea vibaya au kwa watu wengine.
Vilevile upo ushahidi wa kitaalamu unasema kuwa watoto hawa wana uwezekano mkubwa wa kuwa wahalifu na kukosa huruma na upendo kwa binadamu wenzao.
Hakuna mtoto ambaye anatamani kuishi mbali na wazazi wake bali ni safari ya maisha inayowalazimu kuishi katika familia baki.
Ukinuia kumlea mtoto wa binaadamu mwenzio, huna budi kumlea katika usawa na kumpatia haki za msingi ikiwa ni pamoja na mapenzi kama ufanyavyo kwa watoto wako. Hakika, tena kwa mifano iliyopo katika jamii zetu, hawa wakifanikiwa – watakulea uzeeni.

No comments

+255716829257